Thursday, May 22, 2014

WAFANYAKAZI WIZARA YA FEDHA WAASWA KUFANYAKAZI KWA BIDII NA KUJITUMA

Wafanyakazi Wizara ya Fedha wameaswa kufanyakazi kwa bidii na kujituma kwa moyo ili kukuza uchumi wa nchi na taifa liweze kusonga mbele na kufikia malengo yake.  
Kauli hiyo imetolewa na Mgeni Rasmi ambaye pia ni Waziri wa Fedha Saada Mkuya Salum wakati wa kufungua mkutano wa Baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo hivi karibuni jijini Dar es salaam. 
“Mnapokuwa kwenye mkutano wenu mjadili bajeti bila kuwa na woga kwa kutumia weledi wenu mlionao na kutoa ushauri na maoni amabayo yatasaidia kujenga na kuimarisha Wizara katika kutekeleza majukumu yake iliyojipangiakwa kuzingatia uhalisia wa uchumi wa nchi” alisema Waziri Saada.  
Katika mkutano huo, Waziri Saada aliwapongeza wafanyakazi hao kwa kufuata maelekezo ya kuwa na vikao vya baraza la wafanyakazi mara mbili kwa mwaka kulingana na mkataba ambapo lengo lamkutano huo ni kupata taafirifa ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2013/14 pamoja na kupitia na kujadili bajeti ya mwaka 2014/2015. 
Aidha, mkutano wa baraza hilo unafanyika kwa kuzingatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Kikwete na katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue kuitisha vikao kulingana na utaratibu uliowekwa. 
Naye Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Servacius Likwelile akimkaribisha Mgeni Rasmi alisema kuwa mkutano huo ndio una wajibu wa  kupitia na kujadili bajeti ya mwaka uliopita na mwaka ujao wa fedha ambapo bajeti ya Taifa itasomwa Juni 12, 2014. 
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha Adam Malima alisema kuwa moyo na kiini cha hatima nchi ipo mikononi mwa watumishi wa Wizara ya Fedha, hivyo ameahidi kuwa ofisi yake kwa kushrikiana na Naibu Waziri mwenzake Mwigulu Nchemba ipo wazi wakati wote ili kuweza kusukuma maendeleo ya nchi. 
Akimshukuru Mgeni Rasmi kwa niaba ya wajumbe wa mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu Wizara hiyo Elizabeth Nyambibo alisema kuwa wajumbe wamemsikia na watafanya kazi kwa bidii na kuwa wabunifu ikiwa ni pamoja na kuwapa ushirikiano viongozi wao walioteuliwa na Rais ili waendelee kuwa “Majembe” katika Wizara hiyo. 
Mkutano huo ulihudhuriwa na wajumbe kutoka nchi nzima ambao watahakikisha  nchi imefika hatua ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 kulinganana na malengo iliyojiwekea katika mpango mkakati wake.

No comments:

Post a Comment